SERA YA MIKOPO
UTANGULIZI
Chama cha Ushirika wa Akiba na Mikopo VIWANGO SACCOS LTD. kilianzishwa na wafanyakazi wa Shirika la viwango Tanzania (TBS) tarehe 28.04.1986 na kusajiliwa kwa mujibu wa sheria ya Vyama vya Ushirika Na. 15 ya mwaka 1982 ambayo ilifanyiwa maboresho mwaka 1991 na kupewa namba ya usajili PRI-DAR-UBG-MC-2022-1022 na leseni namba MSP3-TCDC/2022-00089.
Sera hii ya mikopo imeandaliwa ili kuweka wazi taratibu za ukopeshaji mikopo kwa wanachama.Vilevile kutoa huduma ya kuweka akiba za kifedha na kupata mikopo wakati inapohitajika.
MADHUMUNI YA SERA YA MIKOPO YA VIWANGO SACCOS LTD
Madhumuni ya sera ni:
(a) kumuwezesha mwanachama kujua taratibu za ukopeshaji na nyaraka zinazohusika.
(b) kumuwezesha mwanachama kujua masharti ya kukidhi kupata mkopo.
(c) kumuwezesha mwanachama kujua aina za mikopo na dhamana zinazokubalika
(d) kumuwezesha mwanachama kujua ukomo wa mikopo ikijumuisha kiwango cha juu cha mkopo kwa mkopaji.
(e) kumuwezesha mwanachama kujua adhabu au ada kwa marejesho yaliyocheleweshwa;
(f) kumuwezesha mwanachama kujua vigezo na masharti ya mkopo kama viwango vya riba, ada, tozo na idadi ya marejesho.
(g) kuiwezesha viwango SACCOS kufanya tathimini ya uwezo wa mkopaji kurejesha mkopo.
(h) kuisaidia kamati ya mikopo kujua ukomo wa juu wa uidhinishaji mikopo.
(i) Kumuwezesha mwanachama kujua masharti ya udhamini wa mkopo
(j) Kumsaidia mwanachama kujua kipindi kinachotolewa kabla ya kuanza kurejesha mkopo
(k) kuiwezesha Viwango SACCOS kuweka utaratibu wa ukusanyaji na ufuatiliaji wa mikopo.
(l) kuiwezesha Viwango SACCOS kuweka vigezo na taratibu za kurekebisha masharti ya mikopo na uhamishaji wa hisa za hiari za mwanachama ikijumuisha idhini na ruhusa
(m) kuiwezesha Viwango SACCOS kuweka kigezo na taratibu za kuidhinisha na kuruhusu kufuta mikopo isiyolipika ufuatiliaji na tathimini ya ubora wa mikopo
(n) kumuwezesha mwachama kujua fomu husika zinazotumika kwa ajili ya maombi ya mkopo
(o) kupunguza hatari ya mikopo mibaya
(p) kujenga imani kwa taasisi za ndani na nje, wanachama na wananchi kwa ujumla.
(q) kuonyesha umakini wa Bodi katika kusimamia shughuli za chama
WALENGWA WA SERA
Walengwa wakuu katika sera hii ni wanachama na watendaji wa VIWANGO SACCOS ambapo Mwanachama mmoja mmoja hukopa kulingana na mahitaji yake na uwezo wake wa kulipa baada ya kuwasilisha fomu ya maombi ya mkopo husika.
MISINGI NA UTARATIBU WA UTOAJI MIKOPO
Misingi ya utoaji wa mikopo kwa wanachama:
a) MTAJI (CAPITAL)
Akiba za wanachama zilizowekwa ndani ya chama zitazingatiwa na kuwa kigezo muhimu cha kutoa mkopo kwa mwanachama.
b) TABIA (CHARACTER)
Tabia ya mkopaji lazima itathiminiwe kulingana na uaminifu wake binafsi na kumbukumbu zake za mikopo. Wanachama, kamati ya usimamizi, kamati ya mikopo au kiongozi yeyote wa chama anayemfahamu mkopaji anaweza kutoa tathimini ya tabia yake katika kurejesha mikopo. Dhamana kubwa iliyopita kiwango cha mkopo isiwe kigezo cha kumpa mkopo mwanachama asiyekuwa na tabia nzuri ya urejeshaji. Wakopaji wapya watatathiminiwa kwa kuzingatia uwezo wao wa akiba/dhamana.
c) HALI (CONDITION)
Hali ya utoaji wa mkopo kwa mwanachama itazingatia mambo ya nje yanayoathiri mkopo wa mwombaji ambayo ni: hali ya uchumi wa nchi, thamani ya fedha, sheria za nchi, hali ya soko la kazi/ajira na mambo mengine yanayoathiri hali ya urejeshaji wa mkopo
d) UWEZO WA MTIRIRIKO WA KIFEDHA (CAPACITY)
Uwezo wa kurejesha mkopo ndiyo kitu cha kwanza cha msingi cha kuangalia katika kutathimini uwezo wa mwanachama kurejesha mkopo anaoomba, katika kuchanganua uwezo wa kurejesha mkopo, vitu vitatu vitazingatiwa:
i. Uwezo wa kurejesha mkopo
ii. Uwezo na matarajio ya kupata marejesho
iii. Hali ya kifedha
e) DHAMANA (COLLATERAL)
i. Dhamana ya kwanza ya mkopo itakuwa ni Akiba, Hisa na Amana za mwanachama husika.
ii. Mwanachama yoyote aliyetimiza mwaka mmoja tangu kujiunga kwake anaweza kumdhamini mwanachama mwenzake pindi achukuapo mkopo,
f) WADHAMINI
Endapo mkopaji atashindwa kulipa deni lake, mdhamini/wadhamini atawajibika kulipa deni la mkopo huo ikiwa ni pamoja na kuzuia akiba, hisa na amana zake chamani.
UTARATIBU WA UTOAJI MIKOPO
1 Mwanachama anayekusudia kupata mkopo atawasilisha maombi kwa kutumia fomu maalum iliyoandaliwa na VIWANGO SACCOS
2 viwango SACCOS Itatoa mikopo isiyozidi miezi 48 kwa ajili ya kuweka mzunguko endelevu wa fedha.
3 Mwanachama mpya ambaye hajathibitishwa kazini atakuwa na haki ya kukopa mkopo wa dharura, Elimu na maalum pekee kulingana na uwezo wake wa kulipa.
4 Mwanachama mpya aliyethibitishwa kazini, pamoja na mikopo mingine atakuwa na haki ya
kukopa hadi mara mbili ya akiba zake kwa mkopo wa maendeleo na mkopo wa gari kulingana
na uwezo wake wa kulipa.
5 Mwanachama aliyethibitishwa kazini na aliyemaliza kulipa mkopo wa maendeleo na mkopo
wa gari awamu ya kwanza kikamilifu atakuwa na haki ya kukopa hadi mara tatu ya akiba zake
kwa mkopo wa maendeleo na mkopo wa gari kulingana na uwezo wake wa kulipa.
6 Maombi ya mikopo ya Maendeleo, ujasiriamali na gari kwa hatua za mwanzo yatapitiwa na
Meneja/Afisa mikopo wa chama na kupelekwa kwenye kikao cha kamati ya Mikopo kwa hatua
ya mwisho ya kujadiliwa na kuidhinishwa.
7 Maombi ya mikopo ya Dharura, maalum na elimu yatapitiwa na kuidhinishwa na Meneja/Afisa
mikopo wa chama na kuwasilishwa kwa Karani wa mahesabu kwa hatua ya malipo.
8 Mikopo ya Maendeleo na gari itapitishwa na kikao cha kamati ya Mikopo kutegemeana na
upatikanaji wa fedha,
9 Maombi ya mikopo yatafuata utaratibu wa “aliyekuja kwanza kupewa kwanza” (First come
first served basis).
10 Ikitokea maombi ya mikopo yanazidi kiasi cha fedha zilizopo, kipaumbele kitatolewa kwa
maombi yenye kiasi kidogo, hata hivyo wakati maombi ya mikopo yatakapojadiliwa hatua
zifuatazo zitafuatwa/ kuzingatiwa
a. Mwanachama ambaye ni mara yake ya kwanza kuomba mkopo
b. Mwanachama ambaye amemaliza kulipa mkopo uliotangulia bila matatizo na kuomba mkopo mwingine
c. Mwanachama ambaye ameshalipa nusu ya mkopo wa awali
11 Maombi ya mkopo yakiidhinishwa fomu ya mkopo itasainiwa na kuonyesha mpango wa
ulipaji (Repayment schedule) pamoja na mkataba wa ukopaji mkopo kati ya mwanachama na
chama. Baada ya hapo malipo yatafanyika kwa hundi au kuhamishwa moja kwa moja kwenye
akaunti ya mkopaji.
RIBA
Viwango vya riba vitapendekezwa na Bodi na kuidhinishwa na Mkutano Mkuu. Mabadiliko ya riba hayataathiri Mikopo iliyotolewa kabla ya mabadiliko.
KINGA DHIDI YA MAJANGA (BIMA YA MIKOPO)
1 Mkopo wa Maendeleo, Mkopo wa gari, mkopo maalum, na mkopo wa dharura utakaotolewa
kwa mkopaji, utalipiwa bima ya asilimia moja (1%) ya kiwango cha mkopo kilichoidhinishwa.
2 Endapo mwanachama atapata ulemavu wa kutojiweza au kufariki, kinga dhidi ya majanga italipa mkopo uliobakia. Akiba, hisa na amana za mwanachama husika zitakabidhiwa kwake mwenyewe au kwa familia/msimamizi wa mirathi wa marehemu.
TOZO LA ADHABU
Rejesho litakalocheleweshwa kwa zaidi ya siku thelathini (30) litatozwa tozo la adhabu ya asilimia tano (5%) kwa kila mwezi unaozidi makubaliano ya marejesho
MASHARTI YA UJUMLA YA UTOAJI WA MKOPO
1 Mkopo utatolewa kwa mwanachama hai wa viwango SACCOS Ltd (aliyetoa kiingilio, aliyenunua
hisa kamili na kuweka akiba ya lazima kila mwezi na kuwa ndani ya viwango SACCOS Ltd kwa
muda usiopungua miezi mitatu toka alipojiunga na chama.
2 Maombi ya mikopo ya Maendeleo na gari ni lazima yaletwe mwezi mmoja kabla.
3 Mikopo ya dharura, elimu na maalum itatolewa siku yoyote ya kazi itakapohitajika
4 Mkopo wowote utakaotolewa kabla ya tarehe 15, marejesho yake yataanza mwezi huohuo na mikopo itakayotolewa baada ya tarehe 15 marejesho yake yataanza mwezi unaofuata.
5 Maombi ya mikopo ya Maendeleo na Gari yatajadiliwa katika vikao halali vitakavyofanywa na kamati ya mikopo ya viwango SACCOS Ltd kwa Quorum inayotakiwa.
6 Kamati ya mikopo itachukua hatua ya kutoidhinisha mkopo ulioombwa hadi hapo masharti yatakapotimia au kuomba taarifa za nyongeza kutoka kwa mwanachama, mwajiri n.k
7 Endapo maombi ya mkopo yamekataliwa au hayakuidhinishwa muombaji atafahamishwa kwa maandishi sababu za kukataa maombi hayo ndani ya siku saba baada ya kikao cha kamati ya mikopo kumalizika.
AINA ZA MIKOPO NA MAREJESHO YAKE
1 MKOPO WA MAENDELEO
Mkopo huu utatolewa kulingana na akiba za mwanachama na utakopeshwa kwa madhumuni ya kufanikisha shughuli za kimaendeleo
Mwanachama ana uhuru wa kukopa kiwango ambacho hakizidi mara tatu (3) ya akiba zake alizowekeza. Hata hivyo, kiwango cha juu cha mkopo kitakuwa TZS 60,000,000/= (Milioni sitini). Hii itategemea zaidi uwezo wa kurejesha ikiwemo kipato cha wa mwanachama husika
Muda wa juu wa marejesho wa mkopo huu ni miezi 48 (miaka 4)
Mwanachama ataruhusiwa kukopa tena iwapo atakuwa amemaliza mkopo wa awali au amesharejesha nusu (1/2) ya mkopo wa awali
Riba ya mkopo huu ni asilimia 12% p.a reducing balance
Mkopo huu utarejeshwa kupitia posho (risk allowance) au mapato mengine halali.
2 MKOPO WA GARI
Mkopo huu utatolewa kulingana na akiba za mwanachama na utakopeshwa kwa madhumuni ya kufanikisha ununuaji wa gari
Mwanachama ana uhuru wa kukopa kiwango ambacho hakizidi mara tatu (3) ya akiba zake alizowekeza. (ikumbukwe akiba zinazozingatiwa kwenye mkopo huu ni akiba bakia baada ya kukopea mkopo wa maendeleo) Hata hivyo, kiwango cha juu cha mkopo kitakuwa TZS 30,000,000/= (Milioni thelathini). Hii itategemea zaidi uwezo wa kurejesha, ikiwemo kipato chake. Mkopo huu utarejeshwa kupitia mshahara
Muda wa juu wa marejesho wa mkopo huu ni miezi 36 (miaka 3)
Mwanachama ataruhusiwa kukopa tena iwapo atakuwa amemaliza mkopo wa awali tu
Riba ya mkopo huu ni asilimia 12% p.a reducing balance
3 MKOPO MAALUM
Mkopo huu utatolewa kwa madhumuni ya kufanikisha shughuli maalum za mwanachama kama sherehe, shughuli binafsi, nk
Kiwango cha juu cha mkopo huu ni TZS 5,000,000/= (Milioni tano)
Muda wa juu wa marejesho ni miezi 18
Riba ya mkopo huu ni asilimia 2.5% kwa mwezi kwa njia reducing balance
4 MKOPO WA DHARURA
Mkopo huu utatolewa kwa madhumuni ya kufanikisha dharura iliyompata mwanachama husika kama vile ugonjwa, ajali nk
Kiwango cha juu cha mkopo huu ni TZS 3,000,000/= (Milioni tatu)
Muda wa juu wa marejesho ni miezi 12 (mwaka mmoja)
Marejesho ya mkopo huu yatapitia makato ya mshahara/allowance ya mwanachama husika kila mwezi. aidha mwanachama anaweza kulipa marejesho ya mkopo wake kutokana na vyanzo vyake vingine halali vya mapato lakini ni lazima zaidi ya ¾ ya marejesho yakatwe toka kwenye posho yake
Riba ya mkopo huu ni asilimia 2% kwa mwezi kwa njia reducing balance
5 MKOPO WA ELIMU
Mkopo huu utatolewa kwa madhumuni ya kufanikisha ulipwaji wa ada ya shule tu
Kiwango cha juu cha mkopo huu ni TZS 1,500,000/= (Milioni moja na laki tano)
Muda wa juu wa marejesho ni miezi 6
Marejesho ya mkopo huu yatapitia makato ya posho ya mwanachama husika kila mwezi. Aidha mwanachama anaweza kulipa marejesho ya mkopo wake kutokana na vyanzo vyake vingine halali vya mapato lakini ni lazima zaidi ya ¾ ya marejesho yakatwe toka kwenye posho yake
Riba ya mkopo huu ni asilimia 2% kwa mwezi kwa njia reducing balance
Mkopo huu hautokuwa na top up
UFUATILIAJI WA MIKOPO NA MATENGO YA MIKOPO MIBAYA
1 KUREJESHA MKOPO
Mwanachama atafanya marejesho ya mkopo na riba kwa kupitia posho na mshahara (kutegemeana na aina ya mkopo) kwa utaratibu na muda uliowekwa
Taarifa juu ya maendeleo ya mikopo zitaandaliwa na kamati ya mikopo kwa kushirikiana na Meneja/Afisa mikopo na kuziwasilisha kwenye vikao vya bodi
Kila mwanachama ana wajibu wa kuhakikisha marejesho ya mikopo yake aliyochukua yanafanyika kama ilivyokubaliwa.
2 MIKOPO/MADENI MABAYA
Madeni mabaya ni yale ambayo yatakuwa yameshindwa kurejeshwa katika kipindi cha miezi 12 na yasiyoweza kurejeshwa
Chama kitatenga asilimia 20% ya faida kila mwaka kwa ajili ya kulipia madeni mabaya
Mikopo iliyocheleweshwa itatambuliwa kuwa imecheleweshwa kulipwa iwapo mambo yafuatayo yatabainika:
1. Iwapo malipo ya marejesho ya mwanachama yatakuwa pungufu ya malipo yaliyotakiwa kulipwa kwa mujibu wa masharti ya mkataba uliosainiwa na mwanachama kipindi anapochukua mkopo
2. Endapo malipo ya marejesho ya mwanachama hayatafanyika ndani ya siku thelathini tangu marejesho hayo kutakiwa kufanyika bila kujali kuwa mkopo uliocheleweshwa ni riba tu au riba na mkopo
3. Iwapo jedwali la marejesho ya mkopo lililopo kwenye fomu ya mikopo halitazingatiwa katika marejesho ya mkopo ya mwanachama
4. Chama kitatayarisha taarifa ya mikopo iliyocheleweshwa ndani ya siku kumi na tano (15) baada ya kuisha kipindi ambacho taarifa hiyo inahusika. Taarifa ya ucheleweshwaji wa mikopo itajumuisha mambo yafuatayo:
i. Jina la mwanachama, anwani yake binafsi
ii. Mkopo halisi uliotolewa na baki ya deni linalodaiwa
iii. Majina ya wadhamini na dhamana yake
iv. Taarifa nyingine zinazohusika kwa mujibu wa fomu ya mkopo
3 UKOKOTOAJI NA UAINISHAJI MIKOPO ILIYOCHELEWESHWA
Chama kitakuwa kinafanya ukokotoaji wa mikopo iliyocheleweshwa kwa kuanzia tarehe ya
mwisho ambayo rejesho la mkopo husika lilifanyika mpaka pale yatakapokuwa yamekamilika.
Mikopo iliyocheleweshwa itakokotolewa kila mwezi na kutolewa taarifa siku ya mwisho wa
mwezi ambapo mikopo hiyo itaainishwa katika makundi yafuatayo:
· Mikopo iliyopo kwenye angalizo-kuchelewa kwa siku 31-90
· Mikopo iliyopo chini ya kiwango-kuchelewa siku 91-180
· Mikopo yenye mashaka-kuchelewa ni siku 181-365
HITIMISHO
11.1 VIWANGO SACCOS inaongozwa kwa kuzingatia sheria ya vyama vya ushirika no 06 ya mwaka 2013 na kanuni zake za mwaka 2015 pamoja na sheria no 10 ya asasi ndogo za fedha ya mwaka 2018 na kanuni zake za mwaka 2019 na miongozo mbalimbali ya Mrajis, masharti ya chama na sera mbalimbali za chama.
11.2 Wanachama wa VIWANGO SACCOS ndiyo walinzi wa taratibu zilizotajwa hapo juu kwa kuzingatia sheria, kuwa wakweli na kutekeleza wajibu wao ili kuboresha huduma za chama.
11.3 Haki ya kukopa aliyonayo mwanachama iendane na wajibu wa kuilinda sera hii ili iwe mwongozo wa shughuli za chama
UTHIBITISHO
Sera hii imethibitishwa, kusomwa, kujadiliwa na kukubaliwa na Mkutano Mkuu wa Wanachama wote wa Viwango SACCOS uliofanyika tarehe 09-12-2023
KAULI MBIU: KOPA KWA BUSARA LIPA KWA WAKATI